Mpango wa Marupurupu kwa Wazee wa Vijiji Kuimarisha Utawala wa Mashinani.
Serikali ya Kitaifa imepongezwa kwa uamuzi wa kuanza kuwalipa wazee wa vijiji marupurupu ya kila mwezi, hatua inayolenga kuimarisha ushirikiano wao na machifu pamoja na vyombo vya usalama katika kutekeleza majukumu ya kiutawala na kudumisha usalama mashinani. Akizungumza Mombasa, Kamishina wa Kaunti hiyo, Mohamed Noor Hassan, amesema marupurupu hayo yatawasaidia wazee wa vijiji kukidhi mahitaji yao ya kimsingi huku yakitambua mchango wao mkubwa katika kuhudumia jamii. Amesema wazee wa vijiji ni kiungo muhimu kati ya wananchi na serikali, wakichangia kwa kiasi kikubwa katika ukusanyaji wa taarifa za kiusalama, utatuzi wa migogoro na kuimarisha utawala bora katika ngazi ya jamii. Wakati huo huo, Kamishina Noor amewataka wazazi kuwa waangalifu na kuwafuatilia watoto wao wakati wa likizo ya shule ili kuwakinga dhidi ya ushawishi wa makundi ya uhalifu na vitendo vingine vinavyoweza kuhatarisha usalama wao. Amesisi...