Mpango wa Marupurupu kwa Wazee wa Vijiji Kuimarisha Utawala wa Mashinani.
Akizungumza Mombasa, Kamishina wa Kaunti hiyo, Mohamed Noor Hassan, amesema marupurupu hayo yatawasaidia wazee wa vijiji kukidhi mahitaji yao ya kimsingi huku yakitambua mchango wao mkubwa katika kuhudumia jamii.
Amesema wazee wa vijiji ni kiungo muhimu kati ya wananchi na serikali, wakichangia kwa kiasi kikubwa katika ukusanyaji wa taarifa za kiusalama, utatuzi wa migogoro na kuimarisha utawala bora katika ngazi ya jamii.
Wakati huo huo, Kamishina Noor amewataka wazazi kuwa waangalifu na kuwafuatilia watoto wao wakati wa likizo ya shule ili kuwakinga dhidi ya ushawishi wa makundi ya uhalifu na vitendo vingine vinavyoweza kuhatarisha usalama wao.
Amesisitiza kuwa vyombo vya usalama vimeimarisha doria na viko tayari kukabiliana kikamilifu na wahalifu watakaojaribu kuvuruga amani.
Mapema wiki hii, Katibu Mkuu wa Wizara ya Usalama wa Ndani, Raymond Omollo, aliongoza kikao cha wadau wa sekta ya usalama katika Kaunti ya Mombasa kuzindua utekelezaji wa mpango huo.
Kikao hicho kilijadili hali ya usalama katika ukanda wa Pwani na kusisitiza umuhimu wa kushirikiana kukabiliana na magenge ya uhalifu, biashara ya dawa za kulevya pamoja na usambazaji wa taarifa za upotoshaji zinazoweza kuhatarisha usalama wa taifa.
Comments
Post a Comment