Serikali Yashinikizwa Kutunga Sheria kudhibiti swala la watu Kutoweka
Wanaharakati wa haki za binadamu na mashirika ya kiraia wametoa wito kwa Serikali na Bunge kutunga sheria inayotambua na kuifanya kuwa kosa la jinai vitendo vya watu kutoweka nchini Kenya. Wito huo umetolewa wakati wa hafla ya kuadhimisha siku ya kimataifa ya uhamasishaji kuhusu watu wanaotoweka, huku wadau wakitaka hatua zaidi zichukuliwe kulinda waathiriwa na familia zao. Wangeshi Grace Kahuria kutoka IMLU, ambaye pia ni mwanachama wa Muungano wa Missing Voices Coalition na mratibu wa Police Reforms Working Group, amesema mamia ya visa vya watu waliopoteza maisha au kutoweka vimeripotiwa nchini kwa miaka kadhaa. Kahuria amesema visa 38 viliripotiwa mwaka 2019, 10 mwaka 2020, 36 mwaka 2021, 22 mwaka 2022, 10 mwaka 2023, zaidi ya 50 mwaka 2024 na visa sita mwaka 2025. Amesema hadi kufikia Agosti mwaka huu, visa 19 tayari vimeripotiwa. ...