Serikali ya kaunti ya Mombasa kuajiri wauguzi 573 kufuatia mgomo unaondelea.

                                 

Kufuatia mgomo wa wauguzi ambao unaendelea nchini na kutatiza shughuli za utoaji huduma za afya Serikali ya kaunti ya Mombasa imetangaza zoezi la kuajiri wauguzi 573 kwa kandarasi ili kuhakikisha huduma za afya zinaendelea kutolewa bila kukatizwa kufuatia mgomo wa kitaifa uliotangazwa na Chama cha Wauguzi Kenya (KNUN).

Akizungumza katika mkutano na wanahabari gavana wa kaunti hiyo Abdulswamad Shariff Nassir amewahakikishia wakazi kuwa hospitali na vituo vyote vya afya vya umma katika kaunti hiyo vitaendelea kutoa huduma licha ya mgomo unaoendelea.

Akiwahakikishia wakaazi wa Mombasa kuwa hakutakuwa na usumbufu wowote wa huduma za afya katika Kaunt hiyo.

Amesema jukumu kuu la serikali ya kaunti ni kulinda maisha ya wananchi na kuhakikisha huduma muhimu zinaendelea kutolewa wakati wote.

                           

"Kwa msingi huo, nimeielekeza Bodi ya Huduma za Umma ya Kaunti kuanza mara moja mchakato wa kuajiri wauguzi 573  kwa kandarasi ili kuhakikisha wananchi wa Mombasa wanaendelea kupata huduma za afya bila kukatizwa," amesema.

Abdulswamad akisema notisi ya mgomo ilitolewa kabla ya wakati, kwa sababu wahusika wa Mkataba wa Makubaliano ya Pamoja bado wanaendelea na mazungumzo. Akiwa na matumaini kuwa mazungumzo hayo yatazaa suluhu ya amani itakayolinda maslahi ya wahudumu wa afya pamoja na wananchi.

Gavana huyo amewataka wauguzi wa Mombasa kuendelea kuwahudumia wananchi huku mazungumzo yakiendelea, akisisitiza kuwa serikali ya kaunti inathamini mchango wao na itaendelea kushughulikia malalamishi yao kupitia mazungumzo na taratibu za kisheria na taasisi husika.

 "Ninawaomba wauguzi wetu wa Mombasa, kwa kuzingatia ushirikiano mzuri tulioujenga kwa miaka mingi, waendelee kuwahudumia wananchi wakati mazungumzo haya yanaendelea. Tunathamini huduma zenu na tumejitolea kushughulikia malalamishi halali kupitia mazungumzo na taratibu zinazofaa za kisheria na kitaasisi," alisema.

Abdulswamad ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Afya katika  Baraza la Magavana (CoG), amesema serikali za kaunti zinatafuta mwongozo wa kisheria kuhusu notisi ya mgomo huo, akieleza kuwa baadhi ya masuala yaliyowasilishwa na chama cha wauguzi bado yanajadiliwa au hayako ndani ya mamlaka ya moja kwa moja ya serikali za kaunti.

Aidha, alisema serikali ya kaunti imepokea taarifa za visa vya watu wachache wanaodaiwa kuwahofisha wahudumu wa afya na kuwazuia wagonjwa kufika katika vituo vya afya vya umma.

Akisema vitendo hivyo havikubaliki, vinakiuka haki ya kikatiba ya wananchi kupata huduma za afya, na havitavumiliwa.

                                  

Gavana akiisisitiza kuwa uamuzi wa kuajiri wauguzi wa ziada unalenga kuhakikisha huduma za afya zinaendelea kutolewa bila kukatizwa na haipaswi kutafsiriwa kama adhabu kwa wahudumu wa afya.

"Hii si hatua ya kuwaadhibu wahudumu wa afya. Ni hatua muhimu ya kuhakikisha wakazi wanaendelea kupata huduma muhimu za afya wakati suala hili likiendelea kushughulikiwa kupitia mazungumzo na mahakama."

Akiahidi kuwa hakuna mgonjwa atakayekosa huduma katika Kaunti ya Mombasa kutokana na mgomo huo uliopangwa.

Chama cha Wauguzi nchini Kenya (KNUN) kimetoa notisi ya mgomo wa kitaifa kikieleza kuwa kuna masuala ambayo hayajapatiwa ufumbuzi, yakiwemo utekelezaji wa Mkataba wa Makubaliano ya Pamoja (CBA), utekelezaji wa makubaliano ya kurejea kazini ya mwaka 2017, miongozo ya maendeleo ya kazi, kuajiriwa rasmi kwa wauguzi wa mpango wa Huduma ya Afya kwa Wote (UHC), pamoja na masuala mengine ya haki za wafanyakazi.


Comments

Popular posts from this blog

Viongozi wa Kidini PPRL Waunga Mkono Agizo la wizara ya elimu la Ratiba ya Masomo Shuleni

Mbunge Feisal Bader Atuhumiwa Kuzuia Msambweni Talent Show Kufanyika Mvindeni Youth Centre.

Kaunti ya Wajir yaandaa Sherehe za Madaraka Day kwa mara ya kwanza tangu Kenya ipate Uhuru.