MWANI WAGEUKA FURSA YA BIASHARA NA SULUHISHO KWA KILIMO UKANDA WA PWANI
Haarakati zimeanzishwa kuhamasisha matumizi ya kichocheo cha ukuaji wa mimea [Biostimulants] vinavyotokana na mwani miongoni mwa wakulima katika maeneo ya Pwani ya Kenya.
Mpango huo unaolenga kushirikisha wakulima katika majaribio
ya bidhaa hizo pia unakusudia kuwasaidia wanawake wanaokusanya mwani kupata
soko la bidhaa zao, huku wakulima wakinufaika na teknolojia inayoweza kuongeza
uzalishaji wa mazao na kuyafanya kustahimili changamoto za mabadiliko ya
tabianchi.
Thierry Bodson, mshirika wa kiufundi kutoka CASCADIA kwa ushirikiano na shirika la Plan International katika mpango huo, amesema
kichocheo cha ukuwaji wa mimea vinaweza kuwa suluhisho la changamoto
zinazowakabili wakulima, hususan wakati wa ukame, kupungua kwa rutuba ya udongo
na magonjwa ya mimea pamoja na mabadiliko ya tabia nchi.
Bodson amesema kichocheo cha ukuaji wa mimea zimetumika na
wakulima kwa vizazi kadhaa, huku tafiti za hivi karibuni zikionyesha kuwa
zinaweza kuwa na manufaa mbalimbali katika uzalishaji wa mazao.
“Biostimulants husaidia mimea kustahimili ukame, kunyonya na
kutumia mbolea kwa ufanisi zaidi, na pia husaidia katika ukuaji wa mizizi ya
mimea,” amesema Bodson.
Akiweka wazi kuwa Lengo ni kuwawezesha wakulima kufuatilia
maendeleo ya mazao na kulinganisha matokeo kabla ya kuamua iwapo bidhaa hizo
zinafaa kwa mazingira yao.
Mpango huo pia unalenga kuimarisha fursa za kiuchumi kwa
wanawake wanaohusika na ukusanyaji wa mwani katika maeneo ya Pwani.
Akisema badala ya mwani kuuzwa kama malighafi pekee, kuna
uwezekano wa kuongezwa thamani kwa kuubadilisha kuwa kichocheo cha ukuaji wa
mimea,hivyo kutengeneza soko jipya kwa vyama vya wanawake vinavyokusanya mwani.
Kampuni ya kutengeneza kichocheo cha ukuaji wa mimea imesema
bidhaa hiyo husaidia mimea kutumia virutubisho na maji kwa ufanisi zaidi, huku
ikisaidia kukabiliana na changamoto za kimazingira kama ukame na chumvi kwenye
udongo.
Muhdhar Mohamed, mwalimu na mjasiriamali wa kampuni ya
Morganic , amesema kichocheo cha ukuaji wa mimea husaidia kuimarisha ukuaji wa mizizi na
kuongeza uwezo wa mimea kunyonya virutubisho baada ya kuwekwa mbolea.
Amesema kampuni yake ina uwezo wa kuzalisha hadi lita 10,000
kwa mwezi, ingawa kwa sasa uzalishaji ni mdogo kutokana na mahitaji ya soko.
Hata hivyo, amesema uhitaji wa kichocheo cha ukuaji wa mimea umeongezeka kwa
karibu asilimia 200 tangu mwaka jana.
Akiipongeza Serikali kwa kuimarisha udhibiti wa pembejeo
bandia kupitia Organic Farm Inputs and Fertilizer Manufacturers Association of
Kenya (OFIMAK).
Amesema kampuni hiyo imefanya majaribio ya kichocheo cha
ukuaji wa mimea [biostimulants] katika mazao mbalimbali yakiwemo mahindi, muhogo,
nyanya na mboga, huku akiamini teknolojia hiyo inaweza kuongeza uzalishaji wa
chakula, hasa maeneo ya Pwani.
Mwangangi kutoka shirika la Plan International amesema biostimulants
husaidia kuimarisha mizizi ya mimea na kuongeza uwezo wake wa kutumia
virutubisho na maji kwa ufanisi, hasa katika maeneo yenye mvua chache na udongo
usio na rutuba.
Akisema mpango huo pia unalenga kuunganisha rasilimali za
bahari, hususan mwani, na kilimo kwa kutengeneza bidhaa zenye thamani zaidi,
hatua inayoweza kuwafungulia wanawake wanaokusanya mwani fursa za soko na
kuwawezesha wakulima kupata suluhisho la ndani dhidi ya changamoto za
mabadiliko ya tabianchi.
Fatuma Masudi, mkulima wa mwani kutoka Shimoni, amesema
alianza kilimo hicho mwaka 2019 bila kufahamu faida zake, lakini kwa sasa
kimekuwa chanzo muhimu cha kipato na kimemwezesha kujenga na kujikimu kimaisha.
Amesema mwani una matumizi mbalimbali, ikiwemo katika bidhaa
za afya na kilimo, huku akieleza kuwa watu wengi wameanza kujiunga na kilimo
hicho kutokana na faida zake za kiuchumi.
Hata hivyo, amesema changamoto kubwa ni baadhi ya wanunuzi
wa awali kuondoka, hali inayowaathiri wakulima.
Fatuma ameiomba Serikali kutafuta masoko ya uhakika na
kuwaunganisha wakulima na wanunuzi ili waweze kuuza mwani kwa bei nzuri.


Comments
Post a Comment