Mpango wa PropelA Waanza Mombasa Kuwawezesha Vijana Kupata Ujuzi wa Ajira.
Mpango wa
PropelA, unaofadhiliwa na Serikali ya Uswisi na unaolenga kupunguza ukosefu wa
ajira miongoni mwa vijana kwa kuwapatia mafunzo ya stadi zinazohitajika katika
soko la ajira, umeanza kutekelezwa katika Kaunti ya Mombasa baada ya kufanikiwa
kwa miaka minne katika kaunti ya Nairobi.
Mkuu wa
Programu kutoka Swisscontact, Jimmy Delyon, amesema mpango huo unawalenga
vijana wenye umri wa kati ya miaka 18 hadi 25, kwa kuwapa mafunzo ya ufundi na
uzoefu wa kazi ili kuongeza nafasi zao za kupata ajira na kujiajiri.
Deylon ameweka
wazi kuwa mpango huo kufika kaunti ya Mombasa umekuja wakati ambapo mahitaji ya
wafanyakazi wenye ujuzi yanaongezeka katika eneo la Pwani, hasa katika sekta ya
ujenzi, huku waajiri wengi wakikabiliwa na uhaba wa mafundi wenye sifa stahiki.
Akiongeza
kuwa mpango wa PropelA unalenga kuwapa vijana ujuzi unaohitajika katika soko
la ajira, kuongeza nafasi zao za kupata kazi na kuchangia ukuaji wa uchumi kwa
kuziba pengo kati ya elimu ya ufundi na mahitaji ya sekta binafsi.
Mkurugenzi
mkuu katika kampuni ya Jupiter Energy Solutions Caroline Kanja amesema kampuni
hiyo imejitolea kukabiliana na uhaba wa wataalamu wenye ujuzi nchini kupitia
ushiriki wake katika mpango wa PropelA, unaolenga kuwapa vijana ujuzi wa
kiufundi na kitaaluma unaohitajika katika soko la ajira.
Kanja amesema
kuwa kampuni hiyo imechangia katika kuandaa mtaala wa mafunzo na kudhamini
wanafunzi ili kuzalisha wataalamu wenye uwezo wa kuajiriwa au kujiajiri.
Amebainisha
kuwa kuajiri wafanyakazi wasio na ujuzi wa kutosha husababisha makosa au
uharibifu mkubwa,kurudiwa kwa kazi na kuchelewesha miradi, jambo linaloathiri
tija na sifa ya kampuni.
Akisisitiza
kuwa uwekezaji katika mafunzo ya ufundi unawapa vijana ujuzi wa vitendo, kipato
cha uhakika na kujiamini, hivyo kuwasaidia kuwa wanajamii wenye tija na
wajasiriamali wenye mafanikio.


.jpeg)

Comments
Post a Comment