KRA Yateketeza Bidhaa Haramu zenye Thamani ya Shilingi Milioni 218.
Mamlaka ya ukusanyaji ushuru nchini (KRA), kwa ushirikiano na taasisi mbalimbali za kiusalama, imeteketeza bidhaa haramu zenye thamani ya Shilingi milioni 218 zilizokamatwa katika operesheni zilizofanyika jijini Nairobi na eneo la Pwani.
Uteketezaji huo ulifanyika kwa wakati mmoja katika kampuni
ya Envirosafe Limited iliyoko EPZ Athi River, Nairobi, na katika eneo maalumu
la Voi, Kaunti ya Taita Taveta. Bidhaa zilizoteketezwa zilijumuisha aina
mbalimbali za bia, pombe kali na maji ya chupa ambazo zilikuwa zimekamatwa
kupitia ukaguzi wa soko na operesheni za utekelezaji.
Uchunguzi umebaini kuwa bidhaa hizo zilikiuka sheria
mbalimbali zinazodhibiti utengenezaji, uagizaji na uuzaji wa bidhaa zinazotozwa
ushuru wa bidhaa. Baadhi ya ukiukaji huo ni pamoja na matumizi ya stempu bandia
za ushuru, matumizi ya stempu zilizobadilishwa au ambazo hazijaamilishwa,
uzalishaji haramu na wazalishaji wasio na leseni, pamoja na mbinu nyingine za
kukwepa kulipa ushuru.
KRA imesema uteketezaji huo unaonyesha dhamira yake ya
kulinda watumiaji, kulinda mapato ya serikali, kuhakikisha ushindani wa haki na
kuvunja mitandao ya biashara haramu inayodhoofisha uchumi wa Kenya.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Meneja Mkuu wa Walipa Kodi
Wadogo na wa Kati, Michael Gichuki, amesema operesheni hiyo ni sehemu ya
mkakati mpana wa KRA wa kulinda wafanyabiashara wanaofuata sheria na kudumisha
uadilifu wa mfumo wa kodi nchini.
Amesema hatua hizo zinalenga kulinda afya, usalama na ustawi
wa kiuchumi wa Wakenya, na si kuwaadhibu wafanyabiashara wanaofuata sheria. Akiongeza
kuwa kuondoa biashara haramu kunasaidia kuunda mazingira salama na yenye
ushindani wa haki kwa wafanyabiashara wanaolipa kodi ipasavyo.
Gichuki amebainisha kuwa biashara haramu ni tishio kubwa kwa
uchumi wa Kenya kwani husababisha upotevu mkubwa wa mapato ya serikali na
kuwaweka watumiaji katika hatari ya kutumia bidhaa zisizokidhi viwango vya
ubora na usalama. Bidhaa nyingi bandia hutengenezwa katika mazingira yasiyo salama
na bila usimamizi wa mamlaka husika.
Aidha, biashara haramu huwadhuru wazalishaji halali kwa
kuleta ushindani usio wa haki, kuhatarisha ajira, kupunguza uwekezaji na
kudhoofisha ukuaji wa viwanda. Kila bidhaa bandia inayouzwa humaanisha serikali
inapoteza mapato ambayo yangetumika kuboresha huduma muhimu kama afya, elimu,
miundombinu na usalama.
Mamalaka hiyo pia imewahimiza wafanyabiashara na wananchi
kutumia Programu ya SOMA Label, inayopatikana bila malipo kupitia Apple App
Store na Google Play Store, ili kuthibitisha uhalali wa stempu za ushuru kabla
ya kununua bidhaa zinazotozwa ushuru.
Mamlaka hiyo imesisitiza kuwa itaendelea kushirikiana na taasisi nyingine katika kupambana na biashara haramu, kulinda watumiaji, kuongeza mapato ya serikali, kuhakikisha ushindani wa haki na kuweka mazingira bora kwa biashara halali kwa mujibu wa sheria za kodi na kanuni za Kenya.


.jpeg)

Comments
Post a Comment