Viongozi wa kiislamu wapongeza Kujumuishwa kwa Duksi na Madrasa Kwenye Mfumo wa Elimu Nchini.



Viongozi wa dini ya Kiislamu kutoka ukanda wa Pwani wamepongeza hatua ya Rais William Ruto ya kutaka mafunzo ya Madrasa na Duksi yajumuishwe katika mfumo wa elimu ya taifa, wakisema hatua hiyo itasaidia kuwajenga wanafunzi kiimani, kuwawezesha kuifahamu dini yao kwa kina kukuza hadhi ya madrasa na duksi.

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini Mombasa, wakiongozwa na Mwenyekiti wa Pwani Patriotic Religious Leaders, Sheikh Abu Qatada, viongozi hao wamesema hatua hiyo itawasaidia wanafunzi kufuata maamrisho ya Mwenyezi Mungu na kuwaepusha na mienendo isiyokubalika kijamii.

Sheikh Abu Qatada amesema kutambuliwa kwa masomo ya dini ya Kiislamu na serikali ni ishara kwamba Rais Ruto ni kiongozi anayethamini dini zote na anatambua umuhimu wa kumcha na kumtumikia Mungu.

Aidha, amesema kuwa kujumuishwa kwa mafunzo ya Madrasa na Duksi kutatoa fursa kwa walimu waliohitimu katika masomo hayo kupata ajira katika shule za umma na za kibinafsi, jambo litakalowawezesha kujikimu kimaisha.

"Tunamshukuru sana Rais kwa kutukumbuka sisi kama jamii ya Waislamu katika taifa hili. Tunampongeza kwa hatua aliyochukua ya kuhakikisha elimu ya Madrasa na Duksi inatambuliwa rasmi katika mfumo wa elimu wa serikali," alisema.

Kwa upande wake, Katibu wa Chuo cha Mafunzo ya Kiislamu cha Sheikh Siraj Rahman, Salim Kifaru, amesema tayari taasisi yao imeanzisha mfumo wa mafunzo unaotambulika kitaifa, ambao utawawezesha wahitimu kupata ajira kupitia vyeti vinavyotambuliwa.

Amesema kauli ya Rais Ruto inafungua njia kwa Madrasa na Duksi kuwa na mtaala unaoendana na mfumo wa elimu nchini, hali itakayowezesha utoaji wa vyeti vinavyotambuliwa na Wizara ya Elimu.

"Hii ni tunu kubwa ambayo Rais Ruto ametupatia sisi Waislamu, na tuna wajibu wa kushirikiana na serikali kuhakikisha hatua hii inatekelezwa kwa manufaa ya wanafunzi na jamii kwa ujumla," alisema.

Naye Mwenyekiti wa Muungano wa Maimamu na Walimu wa Madrasa wa Kilifi Kusini, Sheikh Hassan Mubarak, amesema hatua hiyo ni ya kihistoria na ya maendeleo kwa kuwa itahakikisha ushirikishwaji na upatikanaji sawa wa elimu kwa watoto wote bila ubaguzi.

 

Akitoa wito kwa Wizara ya Elimu kuhakikisha agizo hilo linatekelezwa kikamilifu ili watoto wote waweze kupata elimu bora na inayotambuliwa rasmi.

"Tunashukuru na kupongeza uamuzi huu wa busara uliofanyika kwa wakati mwafaka. Ni hatua yenye manufaa makubwa kwa taifa na kwa vizazi vya sasa na vijavyo," alisema.

Comments

Popular posts from this blog

Viongozi wa Kidini PPRL Waunga Mkono Agizo la wizara ya elimu la Ratiba ya Masomo Shuleni

Mbunge Feisal Bader Atuhumiwa Kuzuia Msambweni Talent Show Kufanyika Mvindeni Youth Centre.

Kaunti ya Wajir yaandaa Sherehe za Madaraka Day kwa mara ya kwanza tangu Kenya ipate Uhuru.