Spika wa bunge la kitaifa Moses Wetang’ula Akemea Siasa za Ukabila na Vurugu.
Spika wa Bunge la Kitaifa, Moses Wetang'ula,
amewataka Wakenya kujiepusha na siasa za ukabila na kukumbatia umoja wa
kitaifa, akisema mustakabali wa nchi unategemea viongozi na wananchi kuweka
maslahi ya taifa mbele badala ya tofauti za kikabila na kisiasa.
Akizungumza katika eneo la Likoni, Kaunti ya
Mombasa, wakati wa hafla ya kuchangisha fedha kwa ajili ya Shirika la Kijamii
la Salute (Salute CBO), Wetang'ula amesema maendeleo ya Kenya yatawezekana
kupitia umoja, mshikamano na kuheshimu demokrasia.
"Nchi yetu ni kubwa kuliko mtu yeyote,
na uongozi hutoka kwa Mungu. Lengo letu linapaswa kuwa kuunganisha taifa
tunapoendelea kuelekea kuwa nchi yenye maendeleo makubwa," alisema.
Amesisitiza kuwa hakuna jamii iliyo kubwa au
ndogo nchini Kenya na kwamba kila jamii ina haki ya kutoa viongozi wake. Aidha,
alitoa wito kwa wanasiasa kudumisha siasa za heshima kwa kushindana kwa amani
wakati wa uchaguzi na kukubali matokeo baada ya uchaguzi.
"Hakuna kabila kubwa wala dogo nchini
Kenya. Kila jamii ina haki ya kuongoza taifa hili. Tunapaswa kudumisha siasa
zenye staha ambapo tunashindana kwa nguvu wakati wa uchaguzi, lakini matokeo
yanapotangazwa, tunakumbatiana na kufanya kazi pamoja kwa manufaa ya
wote," alisema.
Spika huyo pia amekemea tabia inayoshuhudiwa
ambapo baadhi ya wanasiasa wanadaiwa kudhamini na kutumia makundi ya wahuni
kusababisha vurugu za kisiasa, akionya kuwa hali hiyo inahatarisha amani na
utulivu uliopatikana kwa juhudi kubwa.
"Ni jambo la kusikitisha kuona baadhi ya
wanasiasa wakiajiri wahuni kuvuruga amani yetu tuliyoijenga kwa gharama kubwa.
Tunapaswa kukemea vitendo hivyo. Ikiwa wanahitaji wahuni, waajiri watoto wao
wenyewe, si watoto wasio na hatia wa taifa hili," alisema.
Wetang'ula amempongeza aliyekuwa Waziri Mkuu
Raila Odinga kwa kuweka maslahi ya taifa mbele baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka
2022, akisema hatua hiyo ilichangia kuundwa kwa serikali jumuishi inayowapa
viongozi kutoka pande mbalimbali za kisiasa nafasi ya kuhudumia taifa.
Wetangula pia ameeleza matumaini yake kuhusu
mustakabali wa Kenya, akisema nchi iko katika mkondo wa ukuaji endelevu na
ustawi wa kiuchumi. Akisema utawala wa Rais William Ruto umeweka msingi wa
mageuzi ya kiuchumi huku taasisi za kidemokrasia zikiendelea kuimarika.
Naye Spika wa Seneti, Amason Kingi, ameunga
mkono wito wa kukomeshwa kwa siasa za ukabila, akisema eneo la Pwani ni la watu
wa tamaduni mbalimbali na haliwezi kuunga mkono siasa za mgawanyiko wa
kikabila.
"Pwani ni eneo lenye watu wa asili na
tamaduni tofauti. Hilo pekee linatupa sababu ya kuunga mkono serikali jumuishi.
Kenya imepiga hatua kubwa katika kuondoa mfumo wa kale wa kuwagawa wananchi kwa
misingi ya ukabila," alisema.
Kwa upande wake, Waziri wa Madini Hassan Joho
alimshukuru Rais William Ruto kwa kuhakikisha Wakenya wote wanatendewa
maendeleo kwa usawa bila kujali kabila
wala dini.
"Kwa miaka mingi, watu wetu walipuuzwa kiuchumi
na kisiasa. Kwa mara ya kwanza, tumesimama kidete na kukubaliana kwamba sisi
pia tunaweza kuongoza. Huu ni wakati wetu wa kuifanya Kenya kuwa taifa bora
zaidi," alisema.
Mbunge wa Likoni, Mishi
Mboko, alimshukuru Wetang'ula kwa ushauri na uongozi wake, akisema atarudisha
wema huo kwa wakati unaofaa.
"Sisi ni matokeo ya malezi na mwongozo
bora. Tumeazimia kwamba wakati utakapofika, nasi tutawaunga mkono wale
waliotunyanyua. Kwa pamoja tunaamini kuwa taifa letu liko kwenye njia sahihi
kuelekea ustawi," alisema.
.jpeg)
.jpeg)





Comments
Post a Comment