Seneta Miraj Abdillahi Apongeza juhudi za serikali katika Kupambana na Mihadarati Mombasa.
Seneta Mteule katika kaunti ya Mombasa Miraj Abdillahi amepongeza idara za
usalama kwa juhudi zake za kupambana na matumizi ya mihadarati pamoja na
kuimarisha usalama katika Kaunti ya Mombasa, hatua ambayo amesema imechangia
kupungua kwa visa vya uhalifu na utovu wa usalama vilivyokuwa vikishuhudiwa
katika maeneo mbalimbali ya kaunti hiyo. Amesema mafanikio hayo yametokana na
ushirikiano mzuri kati ya vyombo vya usalama na wananchi.
Akizungumza katika eneo bunge la Jomvu wakati wa maadhimisho ya Siku ya
Kimataifa ya Kupambana na Dawa za Kulevya, Miraj amesema ukanda wa Pwani kwa
miaka mingi umekuwa ukikabiliwa na changamoto ya matumizi na biashara ya
mihadarati. Hata hivyo, amebainisha kuwa kupitia ushirikiano kati ya Wizara ya
Usalama wa Ndani, vyombo vya usalama na serikali ya kaunti, hatua kubwa
zimepigwa katika kudhibiti tatizo hilo. Amesema juhudi hizo zimewaokoa vijana
wengi kutoka katika uraibu wa dawa za kulevya na kuwapa fursa ya kujijenga upya
na kuboresha maisha yao.
Aidha, amewapongeza vijana pamoja na mashirika mbalimbali ya kijamii ambao
wamejitolea kuwasaidia wenzao kuachana na matumizi ya dawa za kulevya kupitia
ushauri nasaha, mafunzo ya stadi za maisha na programu za kuwawezesha kiuchumi.
Akisema mchango wao umeleta matumaini kwa vijana wengi waliokuwa wamekata
tamaa.
Seneta huyo pia ametoa pongezi maalum kwa Mkurugenzi wa Shirika la Reachout,
Taib Abdulrahman, kwa kujitolea kwake kupambana na tatizo la mihadarati na
kuwawezesha vijana kupitia programu mbalimbali za urekebishaji na maendeleo.
Akiitaka serikali kutambua na kuunga mkono juhudi zake pamoja na mashirika
mengine yanayofanya kazi ya kuwaokoa vijana dhidi ya matumizi ya dawa za
kulevya.
Miraj pia amempongeza Gavana wa Mombasa kwa juhudi zake za kupambana na
matumizi na usambazaji wa dawa za kulevya, akisema kampeni hizo zimeleta
matokeo chanya. Amewataka vijana kuachana kabisa na matumizi ya mihadarati,
wakisisitiza kuwa kufanya hivyo kutawapa nafasi ya kutimiza ndoto zao,
kujijengea maisha bora na kuchangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.
Vilevile seneta Miraj ameitaka serikali kupeleka huduma za usajili na utoaji wa vyeti vya kuzaliwa
moja kwa moja katika shule za ukanda wa Pwani ili kuwawezesha wanafunzi wengi
kupata vyeti hivyo kwa urahisi. Akisema hatua hiyo itasaidia shule kusajili
wanafunzi ipasavyo na kunufaika na mgao wa fedha unaotolewa na serikali
kulingana na idadi halisi ya wanafunzi.


Comments
Post a Comment