Maadhimisho ya Siku ya Mtoto mwafrika: Viongozi Kilifi watoa Wito wa Kulinda Watoto.
Viongozi wa Kaunti ya Kilifi wametoa wito kwa jamii
kushirikiana katika kuimarisha ulinzi wa watoto na kuhakikisha wanapata haki
zao za msingi, ikiwemo elimu, huduma za afya, maji safi na mazingira salama ya
kuishi.
Wakizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa mwafrika,
viongozi hao walisisitiza kuwa jukumu la kulinda watoto si la serikali pekee,
bali ni wajibu wa kila mwanajamii.
Akiongea katika hafla hiyo naibu Gavana wa Kilifi, Flora
Chibule, amesema maadhimisho hayo yanatoa fursa ya kutafakari wajibu wa pamoja
wa kulinda, kulea na kuwekeza kwa kila mtoto ili kuhakikisha anafikia ndoto
zake.
Akiangazia kaulimbiu ya mwaka huu, “Kuhakikisha Kila Mtoto
wa mwafrika Anapata Huduma ya Maji Safi, Usafi wa Mazingira na Afya ya Usafi,”
Chibule amesema upatikanaji wa maji safi ni haki ya msingi inayostahili heshima
na utu.
Alieleza kuwa ukosefu wa maji safi na huduma bora za usafi
wa mazingira huwanyima watoto muda wa kujifunza na kuwaweka katika hatari ya
maradhi, unyanyasaji na ukatili wa kijinsia wanapolazimika kutembea umbali
mrefu kutafuta maji.
Chibule ameonya kuwa changamoto kama biashara haramu ya
watoto, unyanyasaji wa kijinsia, mimba za utotoni, mila potofu, umaskini na
migogoro ya kifamilia zinaendelea kuhatarisha ustawi wa watoto katika kaunti
hiyo.
“Mtoto wa mwenzako ni mtoto wako. Ulinzi wa mtoto huanza
pale jamii inapochukua hatua za kuhakikisha usalama na ustawi wa watoto wote,”
alisema.
Kwa upande wake, Afisa wa Watoto wa Kaunti ya Kilifi, Kelvin
Mugambi, aliwataka wazazi, walezi na wananchi kwa ujumla kuripoti kwa wakati
visa vyote vya dhuluma na unyanyasaji dhidi ya watoto ili wahusika wachukuliwe
hatua za kisheria.
Mugambi amesema serikali ya kitaifa na ile ya kaunti
zinapaswa kuendelea kuwekeza katika mazingira salama kwa watoto pamoja na
kushughulikia changamoto za upatikanaji wa maji katika maeneo yenye ukame ili
watoto wapate fursa ya kuhudhuria masomo badala ya kutumia muda mwingi kutafuta
maji.
Naye Waziri wa Vijana, Michezo na Huduma za Jamii, Dr Ruth
Dama Masha, aliwataka wazazi na walezi kuimarisha mawasiliano na watoto wao na
kuwapa ushauri nasaha ili kuwasaidia kukabiliana na changamoto mbalimbali,
ikiwemo afya ya akili na msongo wa mawazo.
Ruth pia aliwahimiza watoto kujiepusha na matumizi ya
mihadarati, akisema kuwa yana madhara makubwa kwa afya na yanaweza kuharibu
ndoto na mustakabali wa maisha yao.
Viongozi hao walisisitiza kuwa Serikali ya Kaunti ya Kilifi
itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuimarisha mifumo ya ulinzi wa
watoto, hususan wale wanaoishi na ulemavu, na kuhakikisha watoto wote wanapata
fursa sawa za kutimiza ndoto zao.


.jpeg)


.jpeg)
Comments
Post a Comment