Mombasa yaadhimisha Siku ya Kimataifa ya Baiskeli; Wadau Washinikiza Uimarishaji wa miundombinu kurahisisha uchukuzi.
Mamia ya waendesha baiskeli walijumuika na viongozi wa Kaunti ya Mombasa pamoja na wadau wa sekta ya usafiri kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Baiskeli huku kaunti hiyo ikithibitisha dhamira yake ya kuendeleza miundombinu salama ya waendesha baiskeli na kuhimiza matumizi ya usafiri endelevu.
Maadhimisho hayo yalifanyika wakati ambapo Mombasa
inaendelea kushuhudia maendeleo makubwa katika ujenzi wa njia maalum za
waendesha baiskeli, hatua inayolenga kupunguza msongamano wa magari, kuboresha
afya ya wananchi na kupunguza uzalishaji wa hewa kaa.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo naibu Gavana wa Kaunti ya
Mombasa, Francis Thoya, amesema matumizi ya baiskeli yanazidi kuwa mtindo wa
maisha na suluhisho la changamoto za usafiri zinazokabili kaunti hiyo.
Ameweka wazi kuwa
serikali ya kaunti kwa ushirikiano na wadau mbalimbali tayari imeanza kupanua
miundombinu ya baiskeli kutoka Barabara ya Links kuelekea katikati ya jiji ili
kuwahamasisha wananchi kutumia zaidi usafiri huo.
Thoya pia amesisitiza umuhimu wa baiskeli katika kulinda
mazingira kwa kupunguza uzalishaji wa hewa chafu kutoka kwa magari.
“Mombasa ni kaunti ndogo zaidi nchini Kenya lakini
inaendelea kukua kwa kasi. Eneo ni finyu na msongamano wa magari unaongezeka
kila siku. Ni wakati wa wananchi kuanza kufikiria njia mbadala za
usafiri,ambayo pia itasaidia kulinda mazingira yetu,”
Mkurugenzi Mkuu wa EBee Africa, Maarten Fonteijn, alisema siku hiyo haikuwa tu ya kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Baiskeli bali pia kusherehekea kukamilika kwa awamu ya kwanza ya njia ya waendesha baiskeli katika kaunti hiyo.
Alibainisha kuwa matumizi ya baiskeli ni suluhisho mojawapo
la changamoto ya msongamano wa magari mjini Mombasa kwani yanawawezesha
wananchi kufika maeneo yao kwa haraka huku wakiboresha afya zao.
"Tunafurahia kukamilika Kwa njia ya baiskeli itasaidia
pakubwa pia katika kupunguza msongamani wa magari"
Kwa upande wake, mkurugenzi wa Kanda wa ITDP Africa Claire
Birungi amesema idadi kubwa ya watu waliojitokeza kushiriki hafla hiyo ni
ishara kwamba wananchi wamekubali matumizi ya baiskeli na sasa kilichobaki ni
kuimarisha miundombinu salama ya waendesha baiskeli.
“ Zaidi ya waendesha baiskeli 200 wamejitokeza kuunga mkono
shughuli hii. Tunahitaji kuendelea kuwekeza katika miundombinu salama ya
baiskeli inayounganishwa na mifumo mingine ya usafiri wa umma,”
Wadau hao walieleza kuwa miundombinu bora ya baiskeli
itasaidia watoto kusafiri kwa usalama, kukuza biashara kwa kurahisisha ufikiaji
wa wateja na kuwapa wananchi njia nafuu na salama ya usafiri.
Kwa upande wake meneja wa programu Global Designing Cities
Initiative, Regatu Solomon amesema Mombasa
ni miongoni mwa miji kumi duniani iliyochaguliwa kati ya miji 275 kufaidika na
mpango wa Bloomberg Initiative for Cycling Infrastructure (BICI), unaosaidia
miji kujenga miundombinu salama na jumuishi ya waendesha baiskeli.
“Tunatoa msaada wa kiufundi na kifedha ili kusaidia Mombasa
kutekeleza miundombinu salama ya waendesha baiskeli kwa manufaa ya watumiaji
wote wa barabara,” alisema.
Mombasa inaelekea kuwa miongoni mwa miji inayoongoza katika
kuhamasisha matumizi ya baiskeli kama njia salama, nafuu na endelevu ya
usafiri.






Comments
Post a Comment