Kenya yathibitisha Kuimarisha Usalama wa Baharini Katika Mkutano wa 4 wa Kamati ya Uongozi ya IORIS,Mombasa.

                                                       


 Kenya imethibitisha dhamira yake ya kuimarisha usalama wa baharini na ushirikiano wa kimataifa wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 4 wa Kamati ya Uongozi ya Jukwaa la Indo-Pacific Regional Information Sharing Platform (IORIS) unaofanyika Mombasa.

Washiriki wanatarajiwa kujadili changamoto mbalimbali za usalama wa baharini ikiwemo uharamia, wizi wa kutumia silaha baharini, uvuvi haramu usioripotiwa na usiodhibitiwa (IUU), pamoja na utupaji wa taka na kemikali hatari katika mazingira ya bahari.

                               

Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen amesema kuwa bahari imekuwa mhimili muhimu wa biashara ya kimataifa kwa karne nyingi, zikichangia ukuaji wa uchumi wa mataifa mbalimbali. Hata hivyo, migogoro inayoendelea katika Mashariki ya Kati imeonyesha jinsi usumbufu wa njia za usafiri wa baharini unavyoweza kuathiri uchumi wa dunia na maisha ya watu wengi.

Amesisitiza kuwa ushirikiano wa kimataifa na ubia kama ule unaoendelezwa kupitia mkutano huo ni muhimu katika kulinda rasilimali za pamoja za baharini na kuhakikisha biashara ya kimataifa inaendelea bila vikwazo.

                                         

Kenya pia ilitoa shukrani kwa Umoja wa Ulaya kwa ushirikiano wake wa muda mrefu katika kuimarisha usalama wa baharini kupitia miradi ya kujenga uwezo na kutoa suluhu za vitendo dhidi ya vitisho vya baharini.

Kupitia mpango wa CRIMARIO, taasisi mbalimbali za Kenya zikiwemo Jeshi la Wanamaji la Kenya, Huduma ya Walinzi wa Pwani ya Kenya, Mamlaka ya Bandari Kenya, Mamlaka ya Bahari Kenya pamoja na Kamati ya Kuratibu Operesheni za Udhibiti wa Mipaka (BCOCC), zimekuwa wanachama hai wa jamii ya IORIS.

Jukwaa la IORIS limechangia kwa kiasi kikubwa kuboresha mawasiliano na ubadilishanaji wa taarifa muhimu kati ya taasisi za usalama wa baharini, hivyo kuimarisha ufuatiliaji wa maeneo ya bahari na usalama wa njia za usafiri wa majini.

Maswala mengine yaliyo angaziwa ni maendeleo ya programu ya simu ya Usalama Baharini, iliyobuniwa kwa ushirikiano kati ya Huduma ya Walinzi wa Pwani ya Kenya na CRIMARIO. Programu hiyo imeunganishwa na mfumo wa IORIS na inawawezesha wavuvi pamoja na watumiaji wengine wa bahari kupata taarifa muhimu za usalama na tahadhari kwa wakati.

                                            

Maafisa hao walisema teknolojia hiyo imeongeza uwezo wa Huduma ya Walinzi wa Pwani ya Kenya kufuatilia shughuli baharini na kutoa mwitikio wa haraka dhidi ya vitisho vya kiusalama.

Kenya imesisitiza kuwa iko tayari kuendelea kushirikiana na mataifa na wadau wengine katika kupambana na vitisho vya baharini na kuhakikisha uhuru wa usafiri wa majini unaendelea kulindwa.

Washiriki wa mkutano huo wamehimizwa kutumia fursa hiyo kutathmini mafanikio yaliyopita, kujifunza kutokana na changamoto zilizojitokeza na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha ushirikiano wa baharini siku zijazo.

                                           

Mkutano huo wa siku tatu umeandaliwa kwa ushirikiano kati ya mpango wa Critical Maritime Routes Indo-Pacific (CRIMARIO) unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya na Huduma ya Walinzi wa Pwani ya Kenya (KCGS) na umewaleta pamoja wadau wa sekta ya bahari kujadili njia za kuimarisha usalama wa bahari na ushirikiano wa kikanda na kimataifa.

Mkutano huo unatarajiwa kuhitimishwa kwa mapendekezo yatakayosaidia kuimarisha utawala wa bahari, ushirikiano wa kiusalama na ubadilishanaji wa taarifa katika ukanda wa Indo-Pacific na kwingineko duniani.


Comments

Popular posts from this blog

Viongozi wa Kidini PPRL Waunga Mkono Agizo la wizara ya elimu la Ratiba ya Masomo Shuleni

Mbunge Feisal Bader Atuhumiwa Kuzuia Msambweni Talent Show Kufanyika Mvindeni Youth Centre.

Kaunti ya Wajir yaandaa Sherehe za Madaraka Day kwa mara ya kwanza tangu Kenya ipate Uhuru.