Kenya Yasisitiza Ushirikiano wa Kimataifa katika Kuhifadhi Bahari.
Serikali ya Kenya imetoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuchukua hatua za haraka na madhubuti kulinda mifumo ya ikolojia ya bahari na kuimarisha uchumi samawati wakati viongozi na wadau kutoka mataifa mbalimbali wakikutana katika Our Ocean Conference linalofanyika kaunti ya Mombasa.
Akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi
wa kongamano hilo katika Hoteli ya PrideInn,naibu wa rais Kithure Kindiki amesema
uhusiano wa Afrika na bahari ni wa kihistoria, wa kina na wa kudumu,
akibainisha kuwa pwani, bandari na mifumo ya ikolojia ya bahari imekuwa msingi
wa ustawi wa jamii nyingi kwa karne nyingi kupitia biashara, utamaduni na
uchumi.
Amesema uchumi wa bahari duniani kwa
sasa unakadiriwa kuwa na thamani ya takribani dola trilioni 3.3 za Marekani kwa
mwaka, sawa na asilimia 2.5 ya pato la taifa la dunia, huku ukitarajiwa kufikia
dola trilioni 5.5 ifikapo mwaka 2030 kupitia sekta kama usafirishaji wa majini,
uvuvi, utalii wa pwani, nishati ya baharini na teknolojia ya viumbe wa majini.
Amesisitiza kuwa uchumi samawati
haupaswi kuangazia tu uchimbaji wa rasilimali za bahari, bali pia usimamizi
endelevu ili kuhakikisha mifumo ya ikolojia ya bahari inalindwa kwa manufaa ya
vizazi vijavyo.
Taifa la Kenya limethibitisha upya
kujitolea kwake kutekeleza makubaliano ya kimataifa ya mazingira, yakiwemo
Makubaliano ya Paris, Mfumo wa Kimataifa wa Bayoanuai wa Kunming-Montreal na
lengo la kulinda asilimia 30 ya maeneo ya baharini na pwani ifikapo mwaka 2030.
Aidha, Kenya imeahidi kuharakisha
utekelezaji wa Makubaliano ya BBNJ barani Afrika na kuimarisha juhudi za
kukabiliana na uchafuzi wa plastiki kupitia mikataba ya kimataifa yenye nguvu
za kisheria.
Kiongozi huyo pia ameeleza kuwa
Kenya inaendelea kupanua maeneo ya hifadhi za bahari, kurejesha mikoko na nyasi
za bahari, kuunda ajira za sekta ya baharini, kujenga bandari rafiki kwa
mazingira na kuwekeza katika miradi ya kaboni pamoja na nishati mbadala
inayotokana na bahari.
Amesisitiza kuwa hakuna taifa
linaloweza kukabiliana na changamoto za bahari peke yake, akitoa wito wa
kuimarishwa kwa ushirikiano katika nyanja za ufadhili, teknolojia, ubunifu na
ujenzi wa uwezo.
Kindiki amewataka wajumbe kubadili
ahadi kuwa vitendo na kufanya kongamano hilo kuwa hatua muhimu katika juhudi za
kimataifa za kulinda bahari.
Kongamano hilo limefunguliwa rasmi
kwa wito wa kuimarisha ushirikiano wa kimataifa ili kuhakikisha bahari inakuwa
salama, safi na zenye ustahimilivu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Kongamano hilo linafanyika chini ya
kaulimbiu "Bahari Yetu, Urithi Wetu, Mustakabali Wetu", wakati
ambapo dunia inakabiliwa na changamoto zinazoongezeka za mabadiliko ya tabianchi,
uchafuzi wa mazingira na shughuli za kibinadamu zinazoweka shinikizo kubwa kwa
bahari.


.jpeg)


Comments
Post a Comment