Kamishna wa Mombasa awaonya Wanasiasa dhidi ya Kutumia Wahuni Kuvuruga Mikutano ya Kisiasa.

 

 

Huku maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027 yakizidi kushika kasi, Kamishna wa Kaunti ya Mombasa, Mohamed Nur, ametoa onyo kali kwa wanasiasa wanaotumia magenge ya wahuni na vijana kuvuruga mikutano ya kisiasa ya wapinzani wao au kujifanya maafisa wa usalama.

 Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Madaraka yaliyofanyika katika Uwanja wa Bilima, Kaunti Ndogo ya Kisauni,Nur amesema vyombo vya usalama vinafuatilia kwa karibu shughuli za kisiasa na havitasita kuchukua hatua kali dhidi ya yeyote atakayekiuka sheria.

 Kamishna huyo alisisitiza kuwa kudumisha amani, utulivu na usalama ni jukumu la kila mwananchi, akiongeza kuwa hakuna mtu atakayelindwa kutokana na hatua za kisheria kwa misingi ya hadhi au cheo chake Kwa jamii, ushawishi wa kisiasa au chama anachokiunga mkono.

 Nur alieleza wasiwasi wake kuhusu ongezeko la visa ambapo baadhi ya wanasiasa wanadaiwa kuwatumia vijana na makundi ya wahuni kusababisha vurugu katika mikutano ya kisiasa, akisema tabia hiyo inahatarisha amani, demokrasia na mshikamano wa kitaifa.

 Aliwataka viongozi wa kisiasa kuendesha shughuli zao kwa uwajibikaji na kuheshimu haki za wapinzani wao kufanya mikutano na kuwasiliana na wafuasi wao bila kuingiliwa.

 Aidha, aliwashauri wanasiasa wanaohitaji ulinzi wakati wa shughuli zao kutafuta huduma rasmi za usalama kutoka kwa Jeshi la Polisi badala ya kutegemea wahuni au makundi ambayo hayajaidhinishwa.

 Kamishna huyo pia aliwataka wakazi wa Mombasa kushirikiana na vyombo vya usalama kwa kutoa taarifa kuhusu watu wanaopanga au kushiriki katika vitendo vya uhalifu na vurugu vinavyoweza kuvuruga mikutano ya umma.

 Kauli zake zinajiri wakati shughuli za kisiasa nchini zinaendelea kuongezeka kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027, huku serikali na vyombo vya usalama vikiahidi kuhakikisha kuwa kampeni na mikutano ya kisiasa inafanyika kwa amani, utulivu na kwa kuzingatia sheria za nchi.

Comments

Popular posts from this blog

Viongozi wa Kidini PPRL Waunga Mkono Agizo la wizara ya elimu la Ratiba ya Masomo Shuleni

Mbunge Feisal Bader Atuhumiwa Kuzuia Msambweni Talent Show Kufanyika Mvindeni Youth Centre.

Kaunti ya Wajir yaandaa Sherehe za Madaraka Day kwa mara ya kwanza tangu Kenya ipate Uhuru.