Kamati ya Fedha Yaahidi Kujumuisha Maoni ya Wananchi Katika Miswada ya Kifedha.
Zoezi la ukusanyaji wa maoni ya wananchi na elimu ya uraia kuhusu miswada mbalimbali ya kifedha limekamilika nchini, huku wananchi wakitoa mapendekezo muhimu yanayolenga kuboresha sera za kodi na usimamizi wa uchumi.
Akizungumza
baada ya kukamilika kwa zoezi hilo katika kaunti ya Mombasa, mwenyekiti wa
Kamati ya Fedha na Mipango ya Kitaifa Kuria Kimani amesema shughuli hiyo imefanyika
katika kaunti 15 zilizoko katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwemo Wajir,
Turkana, Kwale, Kilifi, Tana River, Makueni, Kiambu na Nairobi.
Wananchi
wakipata fursa ya kujadili Mswada wa Fedha wa mwaka 2026/27, Mswada wa
Marekebisho ya Benki Kuu ya Kenya (CBK), Mswada wa Marekebisho ya Mamlaka ya
Ukusanyaji Ushuru ya Kenya (KRA) pamoja na Mswada wa Marekebisho ya Hazina ya
Taifa ya Uwekezaji (Sovereign Wealth Fund).
Miongoni mwa
masuala yaliyoibuliwa ni pendekezo la ushuru wa simu za mkononi. Wananchi wakieeleza
kuwa ingawa kuna mpango wa kupunguza kiwango cha ushuru kutoka asilimia 55.5
hadi 50, bado kuna mkanganyiko kuhusu pendekezo la kulipa ushuru wakati wa
kuwasha simu kwa mara ya kwanza. Wengi wakipendekeza ushuru huo ulipwe mara
moja wakati wa kununua simu.
Aidha,
wananchi walitaka wafanyakazi wanaopata mshahara usiozidi Shilingi elfu 30,000 waondolewe
ushuru wa PAYE ili kupunguza gharama ya maisha.
Kamati hiyo
imeahidi kuwasilisha mapendekezo ya marekebisho ya miswada hiyo bungeni wiki
ijayo baada ya kuyajumuisha maoni ya wananchi kote nchini.
Akiongelea
swala la safari za Rais nje ya nchi, kiongozi huyo alisema ziara hizo zina
manufaa ya moja kwa moja kwa uchumi wa taifa kupitia makubaliano ya biashara na
kidiplomasia.
Amesema
ziara ya Iran ilifanikisha makubaliano ya kuuza chai ya Kenya moja kwa moja
katika soko hilo, huku mazungumzo yaliyofanyika Afrika Kusini yakichangia
kuondolewa kwa masharti ya visa kwa Wakenya wanaotembelea nchi hiyo.
Akiongeza
kuwa hatua hizo zinaimarisha pasipoti ya Kenya na kufungua fursa zaidi za
ajira, biashara na utalii kwa wananchi.
Mwenyekiti huyo
amesisitiza kuwa mapendekezo yote yaliyokusanywa yatajadiliwa na kuwasilishwa
kama marekebisho ya sheria husika.
Pia ameahidi
kuwa sauti za wananchi kuhusu ukosefu wa imani kwa viongozi wao zitazingatiwa
katika mijadala ya bunge.
Amesema watachunguza
sababu za kucheleweshwa kwa malipo ya pensheni kwa baadhi ya wastaafu wa
Mamlaka ya Bandari Kenya (KPA).
Kamati hiyo
ilisema michango ya pensheni hukatwa moja kwa moja kutoka mishahara ya
wafanyakazi na kuwekeza, hivyo hakuna sababu ya msingi ya kucheleweshwa kwa
malipo baada ya mfanyakazi kustaafu.
Baada ya
mchakato wa bajeti kukamilika, kamati hiyo inapanga kuwaita wadau husika ili
kutafuta suluhu ya kudumu kwa tatizo hilo ambalo limewaathiri wastaafu wengi wa
Mombasa.




.jpeg)
Comments
Post a Comment