Viongozi kutoka kaunti ya Mombasa wajitokeza kumtetea Hassan Omar Sarai.



Baadhi ya viongozi na wakazi wa Kaunti ya Mombasa wanaendelea kujitokeza kumtetea Katibu Mkuu wa Chama cha UDA, Hassan Omar Sarai, kufuatia semi zake zilizoibua utata.

Hii ni baada baadhi ya viongozi kutoka eneo la Mlima Kenya kushinikiza Katibu mkuu huyo wa UDA ajiuzulu kutoka wadhifa wake kwa madai ya  semi zake zinachochea ukabila.

Wakiongozwa na mwanaharakati wa kisiasa Said Twaha wamesema kuwa kauli za Sarai zilikuwa zinalenga kutetea haki za wakazi wa Pwani waliopokonywa mashamba yao, na wala hazikulenga kuchochea jamii yoyote kama inavyodaiwa na baadhi ya viongozi hao.

Twaha amesema wataendelea kusimama kidete na Katibu Mkuu huyo wa UDA kwa kuwa amekuwa nguzo muhimu ya umoja na mshikamano wa amani katika eneo la Pwani.

Aidha, amemhakikishia Rais kuwa watafanya kila juhudi kuhakikisha chama cha UDA kinapata asilimia 100 ya kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

“Hassan Sarai ameongea kutetea watu wake WA pwani na hakuchochea ukabila,sisi tumeishi Kwa amani tangu jadi. Tunamwambia Rais tunataka Hassan Sarai asibanduliwe katika wadhafa wake”.

                                       

Kwa upande wake, mmoja wa viongozi wa vijana kutoka Kaunti ya Mombasa, Suleiman Hassan, amesema vijana wataendelea kumuunga mkono Sarai na hawatakubali abanduliwe katika wadhifa huo.

Amesema Sarai aliteuliwa na Rais kwa lengo la kuimarisha ujumuishaji wa jamii mbalimbali serikalini na kwamba ameendelea kutekeleza majukumu yake kwa weledi na ufanisi.

“Maneno ya Sarai kujiuzulu tumekataa.katika UDA viti vimegawanywa kuleta ujumuishwaji WA Kila jamii,kutaka kumtoa ni kutuonea”.

Naye Mohamed Yere, mmoja wa viongozi kutoka jamii ya Wasomali katika Kaunti ya Mombasa, amesema kuwa iwapo Sarai ataondolewa katika nafasi yake, wao pia watajiondoa ndani ya chama hicho. 

Amekemea vikali madai kwamba Sarai anachochea ukabila, akisema amekuwa kinara wa kuunganisha jamii tofauti.

“Sisi kama jamii ya Wasomali tumekataa na akitolewa tutatoka na yeye. Sarai hana ukabila wenye ukabila wabaki na ukabila wao”.

Joyce Wairimu amesema kuwa wakazi wa Mombasa wameishi kwa amani na mshikamano kwa miaka mingi bila ubaguzi wa kikabila, na kwamba Sarai amekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha umoja huo.

Kwa upande wake, Halima Omar amesema Sarai ni kiongozi anayeheshimu na kuthamini jamii zote bila kujali kabila, na kwamba amekuwa akifanya kazi kwa misingi ya usawa na ujumuishaji.

Comments

Popular posts from this blog

Viongozi wa Kidini PPRL Waunga Mkono Agizo la wizara ya elimu la Ratiba ya Masomo Shuleni

Mbunge Feisal Bader Atuhumiwa Kuzuia Msambweni Talent Show Kufanyika Mvindeni Youth Centre.

Kaunti ya Wajir yaandaa Sherehe za Madaraka Day kwa mara ya kwanza tangu Kenya ipate Uhuru.