Mwanahamisi Hamadi aadhimisha siku ya usafi wa hedhi na wanafunzi wa kike Likoni.
Mwanahabari maarufu na mwanzilishi wa Waqf wa Taji Langu,Mwanahamisi Hamadi, ameungana na wasichana wa shule mbalimbali za Likoni kuadhimisha siku ya Usafi wa Hedhi Duniani.
Akizungumza katika shule ya msingi ya Shikaadabu,Mwanahamisi amesema kuwa lengo la kampeni hiyo ni kuwapatia wasichana wanaosoma elimu kuhusu hedhi na usafi wa hedhi pamoja na jinsi jamii inaweza kushirikiana kupambana na unyanyapaa unaozunguka suala hilo.
“Umuhimu wa hafla hii hauko tu katika kuwa mpango wa kiafya, bali pia ni hatua muhimu katika kuendeleza heshima na elimu ya mtoto wa kike. Kwa kuhimiza mazungumzo ya wazi na kutoa taarifa muhimu, tunalenga kuwawezesha wavulana na wasichana kwa maarifa yatakayowasaidia kusimamia afya ya hedhi kwa kujiamini tena bila aibu,” alisema mwanahabari huyo.
Mwanahamisi amesema amefurahia kupata nafasi ya kugawa sodo kwa wanafunzi hao ili kuhakikisha kuwa wakati wa hedhi, wasichana wanaweza kushiriki kikamilifu katika masomo yao bila usumbufu.
Kwa upande wao walimu walieleza kuwa ukosefu wa sodo huwafanya wasichana wengi kubaki nyumbani kila mwezi wanapokuwa kwenye hedhi, jambo ambalo huathiri masomo yao. Walisema iwapo tatizo hilo halitashughulikiwa mapema, linaweza kusababisha ongezeko la wasichana wanaoacha shule.
Takriban wanafunzi milioni Moja hukosa kuhudhuria masomo wakati wa hedhi huku wanaoathirika zaidi wakiwa kutoka mashinani.


Comments
Post a Comment